Wednesday, May 7, 2014

Ulinganishi na ulinganuo wa hadithi fupi andishi na rwaya za kiswahili.




Wataalamu mbalimbali wametoa fasili mbalimbali za hadithi fupi andishi kama ifuatavyo:-
Msokile (1992) Anasema, hadithi fupi ni aina ya kazi ya sanaa ya utanzu wa hadithi inayotumia lugha iliyoandikwa katika nathari au iliyo katika masimulizi kama haijaandikwa. Ni wazi kwamba katika fasihi hii inabainisha uwezekano wa hadithi fupi kuwa simulizi au andishi.
Wamitila (2004) Hadithi fupi ni hadithi inayojifunga kwa idadi ndogo ya wahusika wa tukio fulani maalumu inayoonesha mabadiliko katika sehemu na wakati wa matukio au mandhari kwa upana na isiyojiingiza kwenye undani wa wahusika. Hadithi fupi husomeka kwa kipindi kifupi sana.
Kwa ujumla tunaweza kusema kwamba, hadithi fupi andishi ni aina ya kazi andishi ambayo huwa fupi na huangazia wazo moja kwa moja kwa kurejea kisa kimoja. Huwa na wahusika wachache na huchukuwa mda mfupi.
Pia wataalamu mbalimbali wamejjadili (fasili) maana ya riwaya.
Wamitila (2003) anasema, riwaya ni kazi ya kinathari au kibunilizi ambayo huwa na urefu wa kutosha, msuko uliojengeka vizuri wahusika wengi walioendelezwa kwa kina yenye kuchukuwa muda mwingi katika maandalizi kuhusisha mandhri maalumu.
Muhando na Balsidya, Riwaya ni kazi ya kubuni, ni hadithi ambayo hutungwa kufuatana na uwezo wa fanani kuibusha mambo kutokana na mazoea au mazingira yake. Wanaendelea kusema riwaya huanzia maneno elfu thelathini na tano na kuendelea.
Senkoro (2011) anasema, kuwa riwaya kiswahili zilizuka kutokana na maendeleo na mageuzi ya kiutamaduni, uchangamano wa maisha ya kijamii, kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni yalipelekea haja ya kimaudhui zaidi ya ngano na hadithi fupi.
Madumilla (2009) anasema, Riwaya ya kiswahili ilitokana na nathari bunifu simulizi kama vile hadithi, hekana na ngano iliyosimuliwa kwa mdomo.
Kwa ujumla riwaya ya kiswahili ni ile ambayo inafungamana na utamaduni wa jamii ya waswahili wenyewe. Mwanzoni riwaya zilitafsiriwa kwa kiswahili kutoka lugha za kigeni kanma vile kiarabu na kizungu na kufanya riwaya za kiswahili kutokea mfano mfano wa riwaya hizo ni kama vile; Habari za mlima  iliyoandikwa na Shekhe Alibin Hemed (1980)
Sifa za hadithi fupi andishi na riwaya ya kiswahili:-
Hadithi fupi andishi huwa na sifa mbalimbali kama vile, kuwa na wahusika wachache na hawaelezwi kiundani, huwa na maneno machache kuanzia elfu kumi na kuendelea, huwa na kisa kimoja, pia wahusika wake huwa hawatukuzwi, suala la muktadha huwa halipewi kipaombele, na vile vile huwa na matukio machache.
Pa riwaya ya kiswahili huwa na sifa mbalimbali kama vile, masimulizi ya kubuni, huwa na sifa ya uganizi, huwa na urefu wa maneno kuanzia elfu thelathini na tano na kuendelea, pia huwa na mawanda mapana katika vipengele kama vile mandhari, wahusika,lugha na pia huwa na uchangamano kwenye visa, matukio na wahusika.
Chimbuko la hadithi fupi andishi na riwaya ya kiswahili zimechangiwa sana na fani za kijadi kama ngano, sira, tendi, masimulizi ya wasafiri, hekaya n.k na mazingira ya jamii.
Fani za kijadi zilikuwepo kwenye fasihi simulizi na kuanza kuigwa na watunzi mbalimbali kutokana na mabadiliko ya kijamii katika kufikia karne ya 16 zilizagaa kila sehemu.
Kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia na maendeleo ya kiuchumi na ndipo riwaya ya kiswahili na hadithi fupi na zilipoanza.
mfano: Hadithi fupi-siku ya mganga
                                -Ngome ya nafsi
                                -Hadili na nduguye
Mfano wa Hadithi fupi:-
MSAFIRI NA NGAMIA
Msafiri mmoja aliamua kupumzika kutokana na upepo mkali na vumbi la jangwani. Aliamua kukaa ndani ya hema lake hadi hali hiyo ya hewa ibadilike ndipo aendelee na safari yake.
Ngamia wake pale nje alikumbwa na baridi kali hivyo akaamua kuomba hifadhi ndani ya hema la bwana wake. “Bwana nakuomba uniruhusu nitie kichwa changu ndani ya hema nijiepushe na athari za upepo na mavumbi yalioko hapa nje” yule msafiri alikataa na kumweleza kuwa haingewezekana kwani hema lilikuwa dogo lakini Ngamia alimrairai hadi alipokubali.
Ngamia kuona kuwa kichwa chake kiko ndani aliomba aingize shingo yake, akadai shingo yake haitachukuwa nafasi kubwa. Naye msafiri akakubali baadaye akakubaliwa kuingiza hadi nundu yake na hatimaye akaingia wote mzima. Msafiri akatabahi, alikuwa amerushwa nje huku ngamia akidai kuwa wasingeweza kuenea pamoja kwani hema lilikuwa dogo. Basi msafiri akaumia nje huku baridi inamzizima ingawa hema lilikuwa lake.
Hali ya hewa ilipobadilika msafiri alimwambia Ngamia kuwa wangeendelea na safari. Baada ya siku kadhaahali ya hewa ilibadilika, mvua kubwa ikanyesha naye msafiri akatafuta hifadhi ndani ya hema lake licha ya kuwa Ngamia alimbembeleza angalau ajiepushe na baridi. Msafiri alikuwa ameapa kutorudia kosa lake la awali.
Ufuatao ni mlinganisho kati ya hadithi fupi andishi na riwaya ya kiswahili kama ifutavyo:-
Ubunifu; zote ni fani za kubuni hubuniwa makusudi kabisa na mtunzi binafsi ambaye huisanifu na kupanga hadithi yake kwa namna anayotaka mwenyewe. Mfano wa hadithi ya “Msafiri na Ngamia” ni kisa cha kubuniwa na cha kupangwa na kusanifiwa na mtunzi kwa mawazo yake mwenyewe, pia katika riwaya ya kiswahili kama vile “Mfadhili” iliyoandikwa na “Hussen Tuwa” kisa chake ni cha kubuniwa kwani mwandishi ametunga kisa chake kutokana na uhalisia wa jamii yake.
Uhalisia; zote husawiri jamii kama ilivyo mfano katika hadithi ya “Msafiri na Ngamia” imeonekana jinsi mtu anavyopata matatizo kutokana na ukarimu mfano wakoloni walitutawala lakini tuliwakaribisha wenyewe, pia katika riwaya “Mfadhili” imeakisi jamii katika masuala ya mapenzi, ulevi, usaliti. Hivyo basi riwaya ya kiswahili na hadithi fupi andishi zote hulenga uhalisia wa jamii.
Lugha; zote hutumia lugha ya kinathari katika kisa cha Ngamia na Msafiri kimetumia lugha ya mafumbo mfano, Ngamia akimaanisha wageni waliokuja Afrika wakaomba kushirikiana na sisi lakini walipokaribishwa walibadilika na kutuletea matatizo. Msafiri, hawa ni waafrika ambao wamekaribisha wageni (wakoloni). Katika riwaya ya kiswahili (Mfadhili) imejaa tamathali za semi, mafumbo, misemo na nahau, lugha ya picha, Tashbiha mfano “gari liliruka juu kama jiwe”
Msuko; hadithi fupi andishi na riwaya ya kiswahili zote huwa wa matukio uliopangwa kwa namna yenye kuleta mtiririko wa mshikamano wa simulio zima mfano katika kisa kizima cha “Ngamia na Msafiri” kisa kimepangwa kwa mtiririko wenye kuleta mshikamano kuanzia msafiri alipomkaribisha Ngamia hadi msafiri alipofukuzwa kwenye hema lake na kukosa hifadhi. Pia katika riwaya ya mfadhili inaonesha mtiririko mzuri uliosukwa kwa visa na matukio mfano kuanzia mahusiano kati ya Gaddi Bullah na Dania kumuomba Gaddi Bullah msamaha kwani aliweza kumfadhili ini lake, hivyo inaonesha msuko na mtiriko wa tukio zima tangia mwanzo wake hadi hatima yake.
Pia upo mlinganuo uliopo kati ya hadithi fupi andishi na riwaya ya kiswahili kama ifuatavyo:-
Urefu; hadithi fupi andishi kawaida huwa haizidi maneno elfu kumi lakini riwaya ya kiswahili huwa na maneno yasiyopungua elfu thelathini na tano na kuendelea hii ni kwa sababu riwaya huwa na kisa kirefu chenye uhitaji wa maneno mengi na wahusika wengi ili kukamilisha kisa kizima ukilinganisha na hadithi fupi andishi kisa chake ni kifupi hivyo huhitaji pia maneno machache kukamilisha simulizi zima.
Uchangamano; hadithi fupi andishi huwa na muundo sahili usiyochangamana na uliyo na tukio moja tu, mfano katika kisa cha “ Ngamia na Msafiri” tunaona tukio linalozungumziwa ni moja linalomhusu Ngamia na Msafiri hivyo huwa ni muundo wa moja kwa moja lakini katika riwaya ya “Mfadhili” ina muundo changamano kwani hueleza kisa cha Dania na Gadi Bullah.
Wahusika; hawa ni watu, vitu na mahali na miungu katika kazi ya fasihi, katika hadithi fupi andishi huwa na wahusika wachache angalabu mhusika mkuu huwa ni mmoja au wawili na wahusika huwa hawakui tabia zao hudhihirika kutokana na matukio mfano katika hadithi fupi ya “ Ngamia na Msafiri” tunaona kuwa wahusika wawili tu katika kisa kizima lakini katika riwaya ya kiswahili wahusika wanakuwa ni wengi, wahusika wakuu huwa ni zaidi ya wawili na pia wahusika hukua,tabia zao hujenga na husababisha matukio, huwa na wahusika wakuu na wajenzi mfano katika riwaya ya “Mfadili” wahusika wakuu ni Gadi Bullah na Dania na wahusika wengine wajenzi.
Dhamira; hapa tunaona kuwa hadithi fupi andishi huwa na dhamira chache aghalabu dhamira kuu moja Mfano katika hadithi hii ya “Ngamia na Msafiri” wazo kuu ni unyonyaji lakini riwaya ya kiswahili huwa na dhamira kuu na dhamira ndogondogo zinazosaidia kukamilisha wazo kuu mfano katika riwaya ya “Mfadhili” dhamira kuu ni “ Mapenzi na ndoa” na dhamira ndogondogo ni kama vile ulevi, usaliti,, bidii katika kazi na ufanisi, ukarimu hivo dhamira hizi ndogondogo husaidia wazo kuu ili kukamilisha simulizi zima.
Mandhari, hili ni eneo au mahali tukio la kazi ya fasihi simulizi au andishi hufanyika, katika hadithi fupi andishi mandhari huwa na mawanda finyu kiwakati wa kijiografia mfano katika hadithi ya “Msafiri na Ngamia” Mandhari iliyotumika ni ya jangwani mahali alipokuwa amejenga hema lake Msafiri lakini katika riwaya ya kiswahili huwa na mawanda  mapana kiwakati na kijiografia, mfano katika riwaya ya “Mfadhili” mandhari iliyotumika ni ya hotelini, Zanzibar, Arusha na Dar es salaam hivyo huonesha mawanda mapana sana ukilinganisha na mandhari ya hadithi fupi andishi.
Japokuwa kuna utofauti uliopo kati ya riwaya ya kiswahili na hadithi fupi andishi lakini zote zinalenga kuelimisha jamii kwani zote zinazungumzia masuala ya jamii husika kama vile mapenzi na ndoa, usaliti, ulevi na dhuluma na pia riwaya ya kiswahili na hadithi fupi andishi zote zinajikita katika kutoa mafunzo na maadili na pia zinatoa masuluhisho mbalimbali ya migogoro inayoikumba jamii, hususani katika migogoro ya kiuchumi kisiasa na kijamii


MAREJEO
Madumulla J.S (2009), Riwaya ya kiswahili na misingi ya uchambuzi,Nairobi:Sitima printer Ltd.
Mulokozi M.M (1996), Utangulizi wa fasihi ya kiswahili, Dar es salaam: TUKI.
Msokole M.(1992), Misingi ya hadithi fupi, Dar es salaam: Dar es salaam University press.
Samwel M,(2012), Hadithi fupi, Nadharia, Mbinu na mifano, Dodoma: Kusenyanda Tanzania.

No comments:

Post a Comment